WALIMU Wanachama wa Chama cha Kutetea Haki na Maslahi ya Walimu Tanzania (CHAKAMWATA) wamelalamikia kitendo cha baadhi ya Walimu wa Shule za Msingi na Sekondari wanaohamia kutoka Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kuzuiwa kujiunga na chama hicho ambacho kipo kwa mujibu wa sheria.
Wanaotuhumiwa kuwazuia walimu hao ni Wakurugenzi, Maafisa Utumishi Wakuu na Maafisa
Utumishi Wasaidizi wa Halmashauri mbalimbali nchini.
Walimu hao
wanadai kuwa licha ya kujiunga na CHAKAMWATA kwa kufuata hatua zote za
kisheria, Maafisa hao wanaoingia kwenye mfumo wa mishahara yao (LAWSON) na wamekuwa wakikataa kuwaunga CHAKAMWATA walikojiunga badala yake
wanawalazimisha wabaki CWT walikojitoa.
Maafisa hao
wanadaiwa kukataa kuondoa makato ya 2% ya CWT na kuingiza michango ya 1% ya
CHAKAMWATA kwenye mishahara ya Walimu wanaojitoa kutoka CWT na kujiunga na
CHAKAMWATA.
Uchunguzi
uliofanywa na mwandishi wetu umebaini kuwepo kwa hali hiyo ya kuzuiwa kwa
Walimu kujiunga na vyama vingine walivyovichagua kwa hiari yao na hali hii ni
kubwa na iko karibu nchi nzima.Muonekano wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi.
...........................................
Mwandishi
alifanikiwa kuwasiliana na Wakurugenzi Watendaji wa baadhi ya Halmashauri za
Wilaya, Wakurugenzi wa Majiji, Manispaa na Miji, Maafisa Utumishi Wakuu na
Wasaidizi pamoja na baadhi ya Wanasheria wa Serikali wa Halmashauri za Wilaya
ili kujua wanasema nini kuhusu malalamiko ya Walimu dhidi yao.
Mkurugenzi
wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya Justice Kijazi ambaye analalamikiwa na walimu
hao kuwa anakataa kutekeleza maagizo ya kuondoa makato ya 2% ya CWT na
kuingiza michango ya 1% ya CHAKAMWATA kwenye mishahara yao alipopigiwa simu
kujibu madai hayo alisema asingeweza kusema lolote kwa kuwa alikuwa nje ya
ofisi.
Hata hivyo, alimueleza mwandishi wetu kwamba angempatia namba ya simu ya afisa aliyemuachia ofisi kwa wakati huo, lakini hakufanya hivyo. Alipopigiwa tena kukumbushiwa hakupokea na hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa simu ya mkononi (meseji) hakujibu.
Hata hivyo
malalamiko ya Walimu katika jiji hilo
yapo kuanzia Mwezi Machi 2025, muda ambao Mkurugenzi Justice Kijazi
amekuwepo ofisini.
Walimu wapatao 881 wa Halmashauri ya Jiji la
Mbeya wanamlalamikia Mkurugenzi wao kuwa ameyashikilia majina yao kwa zaidi ya
mwaka mmoja na mkurugenzi huyo amewazuia wasiondolewe CWT wala wasiingizwe
CHAKAMWATA tangu mwaka 2025 licha ya walimu hao kukamilisha taratibu zote
zinazohitajika kisheria.
Katika
Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba mkoani Mtwara, Walimu wa Shule za Msingi na
Sekondari wanamlalamikia Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya hiyo, Afisa Utumishi
Mkuu pamoja na Afisa Utumishi Mkuu Msaidizi kwa kukataa kutekeleza maelekezo
yao ya kuondoa makato ya 2% ya CWT na kuingiza michango ya 1% ya CHAKAMWATA
kwenye mishahara yao baada ya kukamilisha hatua zote za kisheria.
Mwandishi
wetu alifanikiwa kupata barua ya mmoja wa walimu waliokataliwa kuhamishwa
kutoka CWT kwenda CHAKAMWATA.
Barua hiyo iliyosainiwa na Fatuma Mabira yenye kumbukumbu namba TDC/PF. 1541/119 ya tarehe 05/11/2025, akimjibu Mwalimu Shabani Ahmadi Napachihi wa Shule ya Msingi Mji Mpya kuwa Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, amekataa kumwondoa Mwalimu huyo kutoka CWT alikojitoa na kumpeleka CHAKAMWATA alikojiunga kwa hiari yake na kwamba kwenye Wilaya yake ya Tandahimba Chama halali cha Walimu ni CWT tu na kwamba Mwalimu huyo ataendelea kukatwa 2% za CWT kwa lazima (ndivyo inavyosema sehemu ya barua hiyo).
Mwandishi wetu alipomtafuta kwa simu
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Mariam Mwanzalima hakuweza kupatikana,
licha ya kupigiwa mara kadhaa.
Wakati
Mabira akimtaka mwandishi wetu awasiliane na Mwanzalima kwa ajili ya kupata
ufafanuzi kuhusu madai hayo alifanikiwa kupata nakala ya barua nyingine
iliyosainiwa na kiongozi huyo.
Barua hiyo yenye kumbukumbu namba J. A. 25/414/02/30 ya tarehe 16 Juni 2025 ilikuwa ikimjibu Mwenyekiti wa CHAKAMWATA wa wilaya hiyo kuwa amekataa kuwaondoa CWT na kufuta makato ya 2% ya CWT kwenye mishahara ya Walimu wote waliohama CWT na kujiunga na CHAKAMWATA na kwamba amekataa kuingiza michango ya 1% ya CHAKAMWATA kwenye mishahara ya walimu hao.
Muonekano wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya Madaba Songea mkoani Ruvuma.
........................................
Madai ya Mkurugenzi huyo kuhusu msimamo wake kwa mujibu wa barua hiyo ya Mwenyekiti wa CHAKAMWATA wa Wilaya ya Tandahimba ni kuwa hayo ni maelekezo ya Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi kupitia Waraka namba 1/2022 wa Msajili wenye kumbukumbu namba DA. 76/380/01/67 wa tarehe 07 Juni 2022, kuwa CHAKAMWATA hakina sifa za kufanyakazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba.
Madai ya
Mkurugenzi huyo yanafanana na madai ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Dk.
Fredrick Sagamiko ambaye kupitia barua yenye kumbukumbu namba HA. 27/294/02/02
ya tarehe 19 Mei 2025, akimjibu Mratibu wa CHAKAMWATA Mkoa wa Dodoma.
Katika barua
hiyo mkurugenzi huyo alikataa kuondoa makato ya 2% ya CWT ili kuingiza michango
ya 1% ya CHAKAMWATA kwenye mishahara ya Walimu 78 waliokuwa wamejitoa kutoka
CWT na kujiunga CHAKAMWATA.
Mkurugenzi
huyo kwenye barua yake anasema hayo ni maagizo kutoka kwa Msajili wa Vyama vya
Wafanyakazi nchini kupitia Waraka wa Msajili namba 1/2022.
Taarifa
zaidi zinasema kuwa unaodaiwa kuwa ni Waraka wa Msajili namba 1/2022 uliandikwa
kwenda kwa Makatibu wakuu wa Vyama vya Wafanyakazi na wala siyo kwenda kwa
Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri za Wilaya.
Hata hivyo,
zipo taarifa kuwa waraka huo unaodaiwa
kutolewa na Msajili unapingana na Sheria ya vyama vya Wafanyakazi na inadaiwa
ulilenga kukibeba Chama cha Walimu Tanzania (CWT) dhidi ya CHAKAMWATA na sasa
unatumika vibaya na wakurugenzi wa halmashauri kuwazuia walimu wote nchini
wasijiunge CHAKAMWATA.
Aidha, kuna
madai kuwa Msajili huyo wa vyama vya Wafanyakazi aliwahi kukipiga marufuku
CHAKAMWATA na baadaye akakifuta kutoka kwenye rejista ya Vyama vya Wafanyakazi
nchini wakati anajua fika kuwa Sheria haimpi mamlaka ya moja kwa moja kufanya
hivyo dhidi ya Vyama vya Wafanyakazi.
Baadaye Msajili alifungua kesi namba 13 ya mwaka 2022 ya kutaka CHAKAMWATA ifutwe ambapo ilifutwa.
CHAKAMWATA
ilipingana na uamuzi huo hivyo, ilikata rufaa katika kesi namba 170 ya mwaka
2023 na hatimaye ikashinda na kurejeshewa usajili wake na Mahakama ya Rufani
Februari 27, 2025.
Katika
Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro madai yaliyotolewa na walimu
waliohamia CHAKAMWATA yanafanana na madai ya Halmashauri nyingine ya kuzuiwa
kujitoa CWT ambapo walimu 200 wamezuiwa.
Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya
..................................
Mwanasheria
wa Serikali wa Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga, Elikarim Tyeah alipoulizwa
kuhusu malalamiko ya Walimu hao alikataa kusema chochote kwa madai kuwa msemaji
wa jambo hilo ni Mkurugenzi.
Hata hivyo,
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga, Saida Mahugu alipopigiwa, simu
yake ilikuwa ikiita bila ya kupokelewa.
Naye, Mkurugenzi
wa Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda, Sophia Kumbuli alipopigiwa simu na
mwandishi wetu kuhusu madai ya walimu
waliotaka kujiunga CHAKAMWATA kuzuiwa kuondoka CWT na kuwa tangu mwezi Julai
2025 mpaka mwezi Machi 2026, zaidi ya Walimu 130 makato yao ya 1% bado
hayajaingizwa, alisema hakuwa na taarifa
hiyo.
Alisema mara
atakaporudi kutoka safari Jijini Dodoma atalifanyia kazi jambo hilo na kila
mwalimu atapewa haki yake.
Aidha,
alisema alikwishaagiza walimu wasiingiliwe kwenye uhuru wao wa kuchagua ni
chama gani cha Walimu wanachotaka kujiunga nacho.
Hata hivyo
mpaka tunapoandika habari hii, Mkurugezi huyo hajayafanyia kazi madai hayo.
Halmashauri
ya Wilaya ya Mbozi walimu waliohamia CHAKAMWATA wamekuwa na malalamiko ya
kuzuiwa kutoka CWT, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani
Songwe, Abdallah Nandonde alipogigiwa simu kwa lengo la kupata ufafanuzi wa
suala hilo, simu iliita bila kupokelewa.
Afisa
Utumishi Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Salum Kalyomunda alipopigiwa na
kuulizwa kuhusu malalamiko ya Walimu zaidi ya 300 wa Shule za Msingi na
Sekondari za Serikali katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ambao amewazuia
kujitoa CWT na kujiunga na CHAKAMWATA tangu mwezi Machi 2025, alisema yuko
kwenye kikao, akitoka atapiga lakini tangu siku hiyo kila alipopigiwa simu
hakupokea.
Katika
Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, inadaiwa walimu zaidi ya 250 waliojitoa CWT na
kujiunga na CHAKAMWATA wamezuiwa, alipogiwa simu Mkurugenzi Mtendaji wa
Halmashauri hiyo Erica Yegella ili
kuzungumzia suala hilo simu yake iliita mara kadhaa bila ya kupokelewa.
Katika Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba mkoani
Mwanza inadaiwa Walimu zaidi ya 170 wamezuiliwa kujitoa CWT na kujiunga na
CHAKAMWATA, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Amon Mkoga, alipopigiwa
simu alisema anawaomba viongozi wa CHAKAMWATA waende ofisini kwake wakazungumze.
Uchunguzi wetu umebaini kuwa Viongozi wa
CHAKAMWATA walipokwenda, Mkurugenzi huyo aliwakabidhi kwa Afisa Utumishi ambaye
anadaiwa kuwazuia walimu hao tangu mwaka 2025, na hakuna utekelezaji wowote
uliofanyika mpaka tunapotoa habari hii.
Kwa upande wa
Halmashauri ya Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, alipopgiwa simu Mkurugenzi
Mtendaji wa Halmashauri hiyo Elizabeth Gumbo na kuelezwa madai ya Maafisa
Utumishi kuitisha kikao cha viongozi na wanachama wa CHAKAMWATA kwa siku mbili
tofauti ambapo pamoja na kuwapa vitisho, maafisa hao wakiongozwa na Afisa Mkuu
Iddi Kalungonji, waliwaambia walimu hao hawatawatoa CWT na kuwaingiza
CHAKAMWATA mpaka watakapohojiwa na Idara ya Utumishi kuhusu kujitoa kwao.
Mkurugenzi huyo alisema hakuwa na taarifa hiyo
na hivyo hawezi kuzungumzia suala hilo mpaka atakapo maliza likizo yake.
Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Nyag’wale mkoani Geita
................................................
Katika
Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza, alipopigiwa simu Afisa
Utumishi Samina Gullam na kuulizwa kuhusu kuwazuia walimu zaidi ya 217
waliojitoa CWT na kujiunga na CHAKAMWATA tangu 2025, alijibu kuwa hawezi
kuzungumza chochote mpaka mwandishi wetu aende ofisi kwake.
Mkurugenzi
wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa, baada ya kuulizwa kama anajua
kuna walimu 48 ambao wamejitoa CWT na wanataka kujiunga na CHAKAMWAKA lakini
hawapewi ushirikiano tangu Machi 2026 wakati kisheria wanapaswa kutekelezewa
matakwa yao ndani ya siku 30 tu.
Mkurugenzi
huyo alisema hajui chochote na kueleza kuwa ni haki ya walimu kujiunga na chama
chochote anachokitaka lakini kuna taratibu ambazo wanapaswa kuzifuata.
Hata hivyo
walimu hao walidai kuwa taratibu hizo tayari walishazifuata ikiwa ni kujaza fomu namba 15 kutoa notisi kwa CWT na kwa mwajiri.
Katika
Wilaya ya Singida DC Walimu waliohamia CHAKAMWATA kutoka CWT walilalamikia
kuzuiwa na Afisa Utumishi wa wilaya hiyo Edwin Mwampamba kwa madai wanasubiri
kupata barua kutoka kwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida.
Mwampamba
alipopigiwa simu na mwandishi wetu ili kutoa ufafanuzi wa madai hayo alikataa
kusema chochote kwa kuwa msemaji ni Mkurugenzi wa halmashauri hiyo,
Mkurugenzi
wa Halmashauri hiyo Stella Chaula alipopigiwa simu ili kutoa ufafanuzi alisema
hajui kuhusu madai hayo na kuwa yupo safarini nje ya Mkoa wa Singida pindi
atakaporudi atafuatilia jambo hilo.
Kwa upande
wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya Florah Luhala
walimu wanamlalamikia kama wilaya zingine ambapo Septemba 26, 2025 aliitisha
kikao cha Vyama vya Walimu nje ya CWT kwa nia ya kuvipiga marufuku ambapo
Katibu Mkuu wa CHAKAMATWA ambaye alihudhuria kikao hicho pasipo kutarajiwa
alimpinga.
Luhala
alipopigiwa simu na mwandishi wetu ili kuzungumzia suala hilo, alisema hakuna
mwalimu ambaye anazuiwa kujiunga na chama kingine inachotakiwa ni kufuata
taratibu zilizopo kama kutoa notisi kwa chama alichotoka ili apate uthibitisho
wa kuhama kwake na pia mwajiri ajulishwe.
Muonekaano wa Jengo la Halmashauri ya Jiji la Dodoma,
.........................................................
Jambo hili
ni kubwa na lina sura ya kitaifa kulingana na uchunguzi uliofanywa na Mwandishi
wetu, kuna Halmashauri nyingi ambazo walimu wamezuiwa kuondoka CWT na kujiunga
CHAKAMWATA licha ya chama hicho kuwepo kisheria.
Msajili wa
Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri Vallence Wambali akizungumzia suala hilo
alikiri kuwepo kwa Waraka huo 1/2022 unaodaiwa kutumiwa na Wakurugenzi kuwazuia Walimu kujiunga na
CHAKAMWATA.
Wambali
alisema Waraka huo unatekelezwa na vyama vyote 35 vilivyo chini ya ofisi yake
na kuwa kujiunga na chama chochote ni hiari ya mfanyakazi husika yeye hahusiki.
“Mwanachama
anapojiunga nacho anapaswa kujisajili mwenyewe kwenye fomu maalumu,” alisema
Wambali
Aidha,
Wambali katika ufafanuzi wake aliwataka
viongozi wa vyama hivyo kufuata katiba na miongozo mbalimbali iliyowekwa pamoja
na kuangalia maslahi ya wanachama, mwajiri na iwapo chama kitakuwa cha kitaifa
kitoe huduma kwa wanachama wake wote.
“Mimi nikiwa
mwangalizi wa vyama hivi nimekuwa nikifanya vikao vya mara kwa mara na viongozi
wa vyama kwa ajili ya kukumbushana mambo mbalimbali ili kuvijenga, lengo
likiwa kuviona vinakua,” alisema Wambali.
Uchunguzi
uliofanywa na mwandishi wetu kwa zaidi ya miezi mitatu sasa umebaini kuwa mpaka
leo hii hakuna hatua zozote zilizochukuliwa na wakurugenzi hao za kuwaruhusu
walimu wanaotaka kuhamia CHAKAMWATA kutoka CWT na kuanza kuwaingizia michango
ya 1% kwenye mishahara yao.
Aidha,
uchunguzi huo ubebaini kuwa Waraka huo ambao Msajili wa vyama vya Wafanyakazi
amekiri kuwa upo na unapaswa kufuatwa na vyama vyote, ndiyo unaolalamikiwa na
Walimu kuwa unapingana na Sheria.
Waraka huo
umedaiwa kutumiwa na Wakurugenzi kuwazuia Walimu kutumia uhuru wao wa kisheria
wa kuchagua vyama vya walimu vya kujiunga navyo kama CHAKAMWATA na unatumika
kuwalazimisha walimu kuwa wanachama wa CWT kwa lazima hata kama hawapendi.
Jambo hilo
la kuwazuia walimu kutojiunga na chama wanachokitaka limedaiwa kuingiliwa na
baadhi ya wakuu wa wilaya na mikoa kuwapinga kujiunga na CHAKAMWATA na chama
wanachokitambua ni CWT.
Mkuu wa Mkoa
wa Singida, Halima Dendego Aprili 18, 2026 alipokuwa kwenye siku ya wadau wa
Elimu mkoani humo iliyofanyika Shule ya Msingi Samamba Kijiji cha Utaho, Kata
ya Kituntu katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi anadaiwa kusema hadharani kuwa
hakitambui CHAKAMWATA bali CWT hatua ambayo imelalamikiwa na walimu.
Hata hivyo,
alipopigiwa simu mara kadhaa kwa nyakati tofauti ili kuzungumzia suala hilo
simu yake ilikuwa ikiita bila kupokelewa na hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa
simu ya mkononi (meseji) hakujibu.
Mkuu wa Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma William Ndile ambaye anadaiwa na walimu hao kuwa alitoa maelekezo kwa wakurugenzi na maafisa Utumishi katika moja ya mikutano yake kuhakikisha zoezi la kuwasajili walimu hao kujiunga na CHAKAMWATA wanalifanya polepole licha ya kujua chama hicho kipo kisheria.
Alipopigiwa simu na mwandishi wetu ili kutoa ufafanuzi wa jambo hilo alisema hakumbuki chochote kuhusu jambo hilo na kuwa anafanya
kazi kwa kufuata barua.
“Sisi
viongozi tunafanya kazi kwa kufuata barua iliyosainiwa kama hao wanaolalamika wanayo wakuoneshe labda
ningekuwa ofisini ningeweza kuangalia kwenye mafaili lakini sasa nipo likizo hivi ni kweli mkuu wa wilaya anaweza kuwazuia walimu wanaotaka kujiunga na chama wanachokitaka,” alihoji Ndile.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Adolf Ndunguru alipopigiwa simu ili kuzungumzia suala hilo, alimtaka mwandishi wetu ampigie Afisa Habari wa TAMISEMI kwa ufafanuzi.
Mwandishi wetu alipompigia simu afisa habari aliyefahamika kwa jina la Projestus Binamungu alisema anayepaswa kuzungumzia jambo hilo ni mkuu wa kitengo cha habari TAMISEMI na kuwa yeye ni afisa habari wa kawaida.
Hata hivyo, Binamungu alisema jambo hilo lilipaswa kushughulikiwa na Katibu Mkuu ambaye ndiyo mwajiri wa walimu.
“Kwa kukusaidia tu, watu ambao wanaweza kulizungumzia suala hilo ni Tume ya Utumishi wa Walimu na ndiyo wanaotetea maslahi yao,” alisema Binamungu.
Aidha, alishangaa kuona jambo ambalo limefika kwa katibu mkuu kurudishwa chini kwa ajili ya kulitolea majibu.
Muonekano wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Bumbuli mkoani Tanga.
...............................










No comments:
Post a Comment