Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Geita ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Mtakuja, ,Constantine Molandi, aliyekuwa kuwa mgeni rasmi, akizungumza kwenye Mahafali ya pili ya kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Shantamine iliyopo Kata ya Mtakuja mkoani Geita.
.......................
Na Joel Maduka, (Singidani Blog) Geita.
UWEPO wa Mabweni katika shule za sekondari
zimeelezwa kuwa ni moja ya kichocheo cha wanafunzi wa kike kufanya vizuri
kwenye masomo yao na kuepukana na vishawishi ambavyo vimekuwa vikiwapelekea
kushindwa kutimiza ndoto zao.
Akizungumza kwenye mahafari ya pili ya kidato cha sita kwenye shule ya
Sekondari ya Shantamine iliyopo kata ya Mtakuja,Halmashauri ya Mji wa
Geita,Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo ambaye pia ni diwani wa Kata
hiyo,Constantine Molandi,amesema suala la uwepo wa mabweni umesaidia kwa kiasi kikubwa
wanafunzi kufanya vizuri kwenye masomo yao kutokana na kupata muda mrefu wa
kujisomea.
“Ukweli uwepo wa mabweni umesaidia kwa kiasi
kikubwa sana kuboresha suala la elimu hususani kwa watoto wa kike ukiangalia
zamani watoto wengi walishindwa kufikia ndoto zao za kimasomo kutokana na
kutembea umbali mrefu kufuata elimu lakini leo hii mfano mzuri ni hapa
shantamine watoto wamekuwa wakifurahia na kufanya vizuri kwenye masomo yao
kutokana na uwepo wa mabweni na sisi kama halmashauri ni kuona tunaongeza Mabweni
mengi zaidi ambayo yatachochea elimu kwa watoto wetu” alisema Molandi.
Nao wazazi na
walimu wameelezea umuhimu wa uwepo wa mabweni shule ambavyo umeendelea
kuwa chachu ya ufaulu mzuri kwa wanafunzi.
“Ufaulu shuleni hapa umekuwa ukiongezeka kila
mwaka kwanza uwepo wa kidato cha tano na sita
kwetu imekuwa ni fursa kwa wanafunzi wa madarasa ya kuanzia kidato cha
kwanza hadi na cha nne wamekuwa
wakitumia kama fursa ya wao kufundishwa masomo ambayo wanaona wanaweza
kufundishwa na wanafunzi wenzao,” alisema Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Kakila Swila,
“Sisi wazazi kwetu imekuwa ni faraja kubwa kuona
watoto wetu wanafanya vizuri kutokana na uwepo wa mabweni ya shule ya Sekondari
Shantamine,” alisema Yohana Mathias kwa niaba ya wazazi.
Nao wanafunzi wa kidato cha Sita wa shule hiyo
ambao wanatarajia kuanza mtihani wao wa kuhitimu kidato cha sita Mei 6, 2024 wameelezea namna walivyojianda
kukabiliana na mtihani huo.
“Tunashukuru kwa maandalizi mazuri ambayo walimu wetu wametupatia tunauhakika wa kufanya vizuri pindi tutakapokwenda kufanya mtihani wetu wa kuhitimu kidato cha sita tunamatumaini makubwa ya kwenda kufanya vizuri,” alisema Elina Dison kwa niaba ya wanafunzi wenzake.
















No comments:
Post a Comment