.......................................
Na Dotto Mwaibale
Leo macho na masikio ya watanzania na wanachama wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) yanaelekezwa Jijini Dodoma ambapo Mwenyekiti wa chama hicho
Taifa Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia kuongoza Kikao cha Kamati Kuu ya
Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kitakachofanyika Ukumbi wa White House jijini
humo.
Ajenda kuu ya kikao hicho ni kufanya Uteuzi wa Mwisho wa
Wagombea nafasi za Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wabunge Viti
Maalum, Baraza la wawakilishi Zanzibar na Baraza la wawakilishi Viti Maalum.
Kikao cha kamati kuu cha chama hicho ndiyo chombo cha mwisho
cha maamuzi ambacho leo kinakwenda
kupeleka furaha kwa watakao teuliwa na vilio kwa watakaoachwa wa nafasi ya ubunge katika kura za
maoni.
Kikao hicho kitamteua mgombea mmoja kwa ajili ya kuingia kwenye
kinyang’anyiro cha ubunge na wagombea wa vyama vingine katika uchaguzi mkuu.
Licha ya wagombea hao kupita kwa kura nyingi za wajumbe
kwenye kura za maoni kikao hicho kitaangalia mambo mbalimbali ya wagombea hao.
Mambo hayo ni kama vile kukubalika kwa wananchi, iwapo mgombea
husika kama alishinda kura hizo kwa njia ya rushwa na mambo mengine.
Lakini licha ya kikao hicho kuwa ndio cha mwisho kwa kutoa
maamuzi kinapaswa pia kuangalia maamuzi ya wananchi waliowachagua wagombea wao
wanaowataka tena kwa kura nyingi vinginevyo kuna hatari ya kutokea changamoto
ya kuwakataa wale watakaoteuliwa na kikao hicho.
Kuna mifano ambayo tumeiona katika maaeneo mengi wakati wa
uteuzi wa wagombea nafasi ya udiwani baada ya vikao vya CCM vya Halmashauri Kuu
za Wilaya na Mikoa kuwapitisha wagombea ambao wananchi hawakuwa chaguo lao.
Wananchi hao walikuwa wakiandamana kwenda ofisi za chama
hicho na kupinga maamuzi ya vikao hivyo vya juu kwa kuwateulia wale ambao hawakuwa
chaguo lao.
Tuliona jinsi vikao hivyo vilivyo lazimika kuketi tena na
kuwarejesha wagombea waliokuwa wakitakiwa na wananchi.
Jambo hilo lilipaswa kuangaliwa kwa umakini kabla ya kuwateua
wagombea hao ambao hawakubaliki na wananchi hatua ambayo itasaidia kupunguza malalamiko
kwa wagombea na wananchi kwa ujumla na muda.
Athari za kuwapekea wananchi viongozi ambao hawawataki ni
kubwa mno kwani wanaweza kukisusia chama na hata kutompa ushirikiano mbunge
ambaye hawakumtaka jambo ambalo litafifisha maendeleo kwenye jimbo husika na Taifa kwa ujumla.
Tuna imani na kikao hicho kutokana na kuwa na timu makini
chini ya Mwenyekiti wake Dkt. Samia hivyo tunatoa rai kwa wagombea kuyaheshimu maamuzi
yatakayofikiwa.
Wagombea wanaaswa kuzingatia utaifa na uzalendo kwani katika
uchaguzi wowote kuna kushinda na kushindwa na kuna mambo ya muhimu yanaangaliwa
kabla ya kuteuliwa na hakuna upendeleo.










No comments:
Post a Comment