SHEIKH NASORO: TAKUKURU MKOA WA SINGIDA MMEWEKA HISTORIA - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Wednesday, March 18, 2026

SHEIKH NASORO: TAKUKURU MKOA WA SINGIDA MMEWEKA HISTORIA

Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro akizungumza kwenye Iftar iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mkoani humo kwa wadau wao Machi 18, 2026.
....................................

Na Dotto Mwaibale, Singida

SHEIKH wa Mkoa wa Singida, Issa Nasoro amesema Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Mkoa wa Singida imeweka hisoria kubwa kwa kuandaa Iftar kwa wadau wake mkoani humo.

Kiongozi huyo mkuu wa dini ya kiislamu mkoani Singida Sheikh Nasoro aliyasema hayo wakati wa hafla ya Iftar iliyoandaliwa na TAKUKURU Mkoa wa Singida iliyofanyika leo Machi 18, 2026 na kuandaliwa na wadau wa taasisi hiyo mkoani hapa.

“TAKUKURU Singida jambo la kufuturisha mlilolifanya halijawahi kufanyika mkoani hapa hakika  mmeweka historia kubwa,” alisema Sheikh Nasoro.

Aidha, Sheikh Nasoro alisema jukumu la kuzuia na kupambana na rushwa  ni la lako na langu hivyo kila mmoja kwa nafasi yake atimize jukumu hilo.

Akizungumzia suala la rushwa Sheik Nasoro alisema hata Mtume Muhammad (SAW) alilikemea na kufika mbali zaidi kwa kueleza alaaniwe mtu aliyetoa na kupokea rushwa na anayefanya hivyo ajitambue yupo katika laana ya Mwenyezi Mungu.

Alisema katika taifa kuwa na watu wenye laana ni angamizo kubwa kwenye jamii hivyo ni vizuri kuikwepa laana hiyo kwa kuacha kufanya vitendo vya rushwa.

Sheikh Nasoro aliongeza kuwa baadhi ya viongozi wa kiislam ambao wamepewa kutoa maamuzi wamekuwa wakifanya vitendo vya rushwa kwa kupokea rushwa na kupindisha haki jambo ambalo siyo zuri mbele ya Mwenyezi Mungu.

Alisema jambo hilo limekuwa likifanyika kwa watoa maamuzi wanaotatua migogoro mbalimbali ikiwemo ya ndoa ambapo wanawake na wanaume wamedaiwa kutoa rushwa ili washinde na kuwaacha wenza wao ili wabaki huru.

“Baada ya kupata ushindi kwa kutoa rushwa baada ya siku kadhaa utakuta ameolewa na yule mtoa maamuzi aliyempa rushwa na kushinda kesi dhidi ya mumewe na vilevile kwa mwanaume kwenda kuoa wakati shauri hilo lingeweza kusuruhishwa kwa haki na maisha yao yakaendelea bila ya kuwa na athari,” alisema Sheikh Nasoro na kuiomba TAKUKURU kulichunguza.

Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Singida, Petro Horombe akizungumza wakati wa Iftar hiyo iliyoandaliwa na taasisi hiyo alisema imelenga kuwahusisha wadau wao wa Mkoa wa Singida.

“Sisi Watumishi wa TAKUKURU ni sehemu ya jamii na ndiyo maana mmekuwa mkituona tukifanyakazi na jamii ikiwa ni pamoja na kutoa misaada mbalimbali ya kijamii na Iftar hii ni sehemu ya matendo tunayofanya,” alisema Horombe.

Mgeni rasmi wa Iftar  hiyo Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Thomas Apson alisema katika utumishi wake wa miaka saba kwa nafasi ya ukuu wa wilaya na miaka mitano ya ubunge hajawahi kuona upendo wa namna hiyo.

“Sijawahi kuona upendo wa aina hii waliotufanyia hawa ndugu zetu wa TAKUKURU kwani wangeweza kujifanyia wenyewe lakini wakaona vizuri watushirikishe tunashukuru sana,” alisema Apson.

Apson alisema suala la mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani la muhimu sana na kuwa linatukumbusha uwepo wa Mwenyezi Mungu na majukumu ya Uislaam kama amani, kusamehana, kufanya dua na kufuata maandiko yaliyopo kwenye Quran,” alisema Apson.

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi mkoani Singida ambaye alikuwa mgeni rasmi Thomas Apson, akizungumza kwenye Iftar hiyo.

Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Singida, Petro Horombe akizungumza wakati wa hafla ya Iftar iliyoandaliwa na taasisi hiyo kwa wadau wake.

Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye Iftar hiyo.

Wadau wa TAKUKURU Mkoa wa Singida wakiwa kwenye hafla hiyo 


 
Iftar ikiendelea
Picha ya pamoja

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad