𝗦𝗔𝗟𝗢𝗠𝗘: 𝗡𝗚𝗨𝗭𝗢 𝗭𝗔 𝗭𝗘𝗚𝗘 𝗡𝗔 𝗖𝗛𝗨𝗠𝗔 𝗞𝗨𝗧𝗨𝗠𝗜𝗞𝗔 𝗞𝗨𝗞𝗔𝗕𝗜𝗟𝗜 𝗖𝗛𝗔𝗡𝗚𝗔𝗠𝗢𝗧𝗢 𝗬𝗔 𝗞𝗨𝗔𝗡𝗚𝗨𝗞𝗔 𝗞𝗪𝗔 𝗡𝗚𝗨𝗭𝗢 𝗭𝗔 𝗨𝗠𝗘𝗠𝗘 𝗭𝗔 𝗠𝗜𝗧𝗜. - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Saturday, May 23, 2026

𝗦𝗔𝗟𝗢𝗠𝗘: 𝗡𝗚𝗨𝗭𝗢 𝗭𝗔 𝗭𝗘𝗚𝗘 𝗡𝗔 𝗖𝗛𝗨𝗠𝗔 𝗞𝗨𝗧𝗨𝗠𝗜𝗞𝗔 𝗞𝗨𝗞𝗔𝗕𝗜𝗟𝗜 𝗖𝗛𝗔𝗡𝗚𝗔𝗠𝗢𝗧𝗢 𝗬𝗔 𝗞𝗨𝗔𝗡𝗚𝗨𝗞𝗔 𝗞𝗪𝗔 𝗡𝗚𝗨𝗭𝗢 𝗭𝗔 𝗨𝗠𝗘𝗠𝗘 𝗭𝗔 𝗠𝗜𝗧𝗜.

NAIBU Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kubadilisha nguzo chakavu kwa kuweka nguzo imara zaidi, zikiwemo nguzo za zege na chuma, pamoja na kuimarisha misingi ya nguzo katika maeneo yenye udongo laini ili kukabili changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme.

Salome ameeleza hayo leo, Mei 22, 2026, Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mhe. Sara Msafiri Ally, Mbunge wa Mvomero, aliyetaka kujua ni lini Serikali itatatua changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme katika Tarafa ya Mgeta.

Akijibu swali hilo, Salome amesema Serikali inatambua uwepo wa changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme katika baadhi ya maeneo ya Tarafa ya Mgeta kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo mvua nyingi, uwepo wa udongo usiohimilivu pamoja na uchakavu wa baadhi ya nguzo.

Amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa miundombinu ya umeme ili kubaini na kushughulikia changamoto hizo mapema pindi zinapojitokeza.

Aidha, Salome amefafanua kuwa Serikali kupitia Wizara ya Nishati imetenga bajeti maalum ya kubadilisha nguzo za miti katika maeneo yote yenye unyevunyevu pamoja na maeneo yenye shughuli mbalimbali za kibinadamu.

Kadhalika, ametoa wito kwa wananchi kuacha matumizi mabaya ya ardhi, ikiwemo kuchoma moto ovyo mashambani, jambo ambalo limekuwa likiathiri miundombinu ya umeme kwa kuunguza nguzo za umeme.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad