ELR, DNATA WAADHIMISHA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA KWA ZIARA YA KIELIMU ZANZIBAR - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Thursday, July 2, 2026

ELR, DNATA WAADHIMISHA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA KWA ZIARA YA KIELIMU ZANZIBAR


Viongozi wa  Kampuni za Emirates Leisure Retail Zanzibar (ELR), DNATA, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA), Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Msingi Fukuchani wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa ziara ya kielimu walioifanya Juni 30, 2026 Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume jikiwa moja la tukio katika Kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika.

..............................

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

KATIKA kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika inayoadhimishwa kila mwaka Juni 16, Kampuni ya Emirates Leisure Retail Zanzibar (ELR), kwa kushirikiana na Kampuni ya DNATA na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA), wamefanikisha ziara ya kielimu kwa wanafunzi 50 pamoja na walimu watatu wa Shule ya Msingi Fukuchani iliofanywa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.

Ziara hiyo ililenga kuwapa wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa katika uwanja wa ndege, ikiwemo huduma za abiria, usalama wa viwanja vya ndege, pamoja na kuwafahamisha kuhusu fursa mbalimbali za ajira na taaluma katika sekta ya usafiri wa anga.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mratibu wa ziara hiyo ambaye pia ni Afisa Utawala Msaidizi wa Emirates Leisure Retail Zanzibar, Hussein Ramadhani Layya (Msokolo), alisema kuwa maadhimisho hayo yalikuwa na lengo la kuwapa watoto elimu, motisha na uzoefu wa vitendo unaoweza kuwasaidia kufikia ndoto zao za baadaye.

"Ni faraja kubwa kuona tabasamu na furaha za watoto hawa. Tunaamini kuwa kuwapatia nafasi ya kujifunza nje ya darasa kunawajengea uelewa mpana, kujiamini na kuwahamasisha kufikia ndoto zao. Kama kampuni, tunaamini kuwa watoto ni hazina ya taifa, hivyo kuwekeza katika elimu na maendeleo yao ni kuwekeza katika mustakabali wa Zanzibar na Afrika kwa ujumla," alisema Layya.

Kwa upande wao, viongozi wa Emirates Leisure Retail Zanzibar (ELR) na DNAATA walisema kuwa kampuni hizo zitaendelea kutekeleza wajibu wake kwa jamii kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuimarisha elimu, afya na ustawi wa jamii.

Viongozi hao kwa nyakaati tofaauti walieleza kuwa shughuli hizo ni sehemu ya utamaduni wa kampuni hizo wa kurejesha kwa jamii na kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuboresha elimu, malezi na ustawi wa watoto.

Aidha, viongozi hao walisisitiza kuwa ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi za umma una mchango mkubwa katika kujenga jamii yenye elimu bora na fursa sawa kwa watoto wote.

Viongozi hao waliahidi kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa jamii.

Mbali na ziara ya kielimu, Emirates Leisure Retail Zanzibar (ELR) na DNATA waliwezesha ziara hiyo kwa kutoa usafiri, chakula na zawadi mbalimbali kwa wanafunzi ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo. Hatua hiyo ilihakikisha watoto wote walipata fursa ya kujifunza, kula na kufurahia siku hiyo katika mazingira ya upendo, mshikamano na kujali.

Shughuli hiyo ilionesha dhamira ya kampuni hizo ya kuendelea kutekeleza programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR), sambamba na kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha elimu, malezi bora na ustawi wa watoto. ELR na DNATA zimesisitiza kuwa zitaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa jamii na kuchangia maendeleo endelevu ya Zanzibar.

Shukrani maalumu zilitolewa kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA), uongozi wa Shule ya Msingi Fukuchani, walimu, wazazi na wadau wote waliochangia kufanikisha ziara hiyo ya kielimu.

Ziara hiyo ilihitimishwa kwa wanafunzi kutembelea maeneo mbalimbali ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, ambapo walipata mafunzo na maelezo kutoka kwa wataalamu wa sekta ya usafiri wa anga kuhusu shughuli mbalimbali zinazofanyika uwanjani. Wanafunzi walijifunza kwa vitendo namna uwanja wa ndege unavyofanya kazi na umuhimu wa kila idara katika kuhakikisha usalama na utoaji wa huduma bora kwa wasafiri.

Maadhimisho hayo yalimalizika kwa watoto kurejea shuleni wakiwa na furaha, maarifa mapya na hamasa ya kuendelea kujifunza kwa bidii ili kutimiza ndoto zao za baadaye. Tukio hilo limeendelea kudhihirisha dhamira ya Emirates Leisure Retail Zanzibar (ELR), DNATA na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA) ya kuwekeza katika elimu, malezi na ustawi wa watoto kupitia ushirikiano imara na jamii, kwa kuamini kuwa watoto wa leo ndio viongozi na wataalamu wa kesho. 

KUHUSU SIKU YA MTOTO WA AFRIKA: HISTORIA YA APARTHEID, VIONGOZI WA UKOMBOZI WA AFRIKA NA WITO WA KUPINGA XENOPHOBIA

Kila mwaka tarehe 16 Juni, Bara la Afrika huadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, siku muhimu ya kumbukumbu, elimu na tafakuri kuhusu haki za watoto na historia ya mapambano ya Waafrika dhidi ya ubaguzi na ukandamizaji.

Siku hii ilianzishwa rasmi mwaka 1991 na Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), ambao sasa ni Umoja wa Afrika (AU), ikiwa ni heshima kwa watoto waliopoteza maisha katika maandamano ya Soweto nchini Afrika Kusini mwaka 1976.

1. HISTORIA YA SOWETO NA APARTHEID

Mnamo tarehe 16 Juni 1976, maelfu ya wanafunzi wa Soweto waliandamana kwa amani wakipinga mfumo wa Apartheid, ambao uliwabagua Waafrika kwa misingi ya rangi na kuwanyima haki za msingi.

Wanafunzi hao walipinga uamuzi wa serikali uliowalazimisha kutumia lugha ya Kiafrikaans kama lugha ya kufundishia, wakidai elimu bora, usawa na heshima kwa utu wao.

Badala ya kusikilizwa, polisi wa serikali ya Apartheid waliwavamia kwa risasi na mabomu ya machozi. Watoto wengi waliuawa, kujeruhiwa na wengine kukamatwa. Tukio hilo liliibua hasira na huruma duniani na kuwa alama ya mapambano ya haki za binadamu.

2. VIONGOZI WA UKOMBOZI WA AFRIKA

Mapambano dhidi ya ukoloni na ubaguzi hayakuishia Afrika Kusini pekee, bali yalienea katika bara lote la Afrika. Viongozi mbalimbali walijitokeza kuongoza harakati za ukombozi, miongoni mwao wakiwa:

Kwame Nkrumah – Ghana

Julius Nyerere – Tanzania

Jomo Kenyatta – Kenya

Patrice Lumumba – DR Congo

Ahmed Sékou Touré – Guinea

Samora Machel – Msumbiji

Agostinho Neto – Angola

Amílcar Cabral

Kenneth Kaunda – Zambia

Robert Mugabe – Zimbabwe

Joshua Nkomo – Zimbabwe

Sam Nujoma – Namibia

Nelson Mandela – Afrika Kusini

Oliver Tambo – Afrika Kusini

Walter Sisulu – Afrika Kusini

Steve Biko – Afrika Kusini

Desmond Tutu – Afrika Kusini

Thomas Sankara – Burkina Faso

Haile Selassie – Ethiopia

Viongozi hawa walikuwa na mchango mkubwa katika harakati za ukombozi na kuimarisha mshikamano wa Waafrika kupitia dhana ya Pan-Africanism.

3. ELIMU, UKOMBOZI NA USTAWI WA MTOTO

Leo hii, Siku ya Mtoto wa Afrika imekuwa zaidi ya kumbukumbu ya historia. Ni siku ya kuwakumbusha viongozi, jamii na taasisi zote kwamba watoto wanahitaji:

Elimu bora na jumuishi

Huduma za afya na lishe

Ulinzi dhidi ya ukatili na unyanyasaji

Mazingira salama ya kukua na kujifunza

Haki ya kushiriki katika maamuzi yanayowahusu

Katika kuadhimisha siku hiyo, Emirates Leisure Retail Zanzibar (ELR) kwa kushirikiana na dnata na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA) waliandaa ziara ya kielimu kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Fukuchani katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.

Ziara hiyo iliwapa wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu huduma za usafiri wa anga, usalama wa viwanja vya ndege na fursa za ajira katika sekta hiyo.

Kwa mujibu wa waandaaji, imekuwa ni utamaduni wa ELR na dnata kushirikiana na jamii kupitia programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR) zinazolenga kuimarisha elimu, afya na ustawi wa jamii.

4. WITO DHIDI YA XENOPHOBIA

Licha ya ushindi dhidi ya Apartheid, Afrika Kusini bado inakabiliwa na changamoto ya xenophobia, yaani chuki dhidi ya wageni kutoka mataifa mengine ya Afrika.

Sababu zake ni pamoja na ukosefu wa ajira, umasikini, ushindani wa rasilimali na taarifa za upotoshaji. Hata hivyo, historia inaonyesha kuwa wakati wa mapambano ya uhuru, mataifa mengi ya Afrika yaliwapa hifadhi na msaada wapigania uhuru wa Afrika Kusini.

Hivyo basi, xenophobia inapingana na historia ya mshikamano wa Waafrika na inapaswa kulaaniwa na kila mwenye nia ya kuona Afrika yenye amani na umoja.

HITIMISHO

Siku ya Mtoto wa Afrika ni zaidi ya kumbukumbu ya kihistoria. Ni somo kwa jamii kwamba uhuru, haki na maendeleo haviji bila mshikamano.

Kwa kuenzi watoto wa Soweto, kuwaheshimu viongozi wa ukombozi wa Afrika na kupinga ubaguzi wa aina yoyote, tunaweza kujenga Afrika yenye amani, usawa na matumaini kwa vizazi vijavyo.

Picha ya paamoja wakati wa ziara hiyo.

Taarifa hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990.
 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad