𝐒𝐄𝐑𝐈𝐊𝐀𝐋𝐈 𝐘𝐀𝐖𝐄𝐊𝐄𝐙𝐀 𝐁𝐈𝐋𝐈𝐎𝐍𝐈 𝟔𝟕.𝟗 𝐓𝐈𝐀, 𝐊𝐀𝐌𝐏𝐀𝐒𝐈 𝐙𝐀𝐅𝐈𝐊𝐈𝐀 𝐍𝐀𝐍𝐄 - SINGIDANIBLOG

Habari za Hivi Punde

Post Top Ad

Monday, September 7, 2026

𝐒𝐄𝐑𝐈𝐊𝐀𝐋𝐈 𝐘𝐀𝐖𝐄𝐊𝐄𝐙𝐀 𝐁𝐈𝐋𝐈𝐎𝐍𝐈 𝟔𝟕.𝟗 𝐓𝐈𝐀, 𝐊𝐀𝐌𝐏𝐀𝐒𝐈 𝐙𝐀𝐅𝐈𝐊𝐈𝐀 𝐍𝐀𝐍𝐄

Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Prof. William Amos Pallangyo, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Septemba 07, 2026, katika ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO, kuhusu utekelezaji wa Taasisi hiyo katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/26 na mwelekeo wa 2026/27.

----------------------

Serikali imewekeza jumla ya Shilingi bilioni 67.9 katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) katika kipindi cha miaka mitano ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Katika Kampasi ya Mwanza, jengo la taaluma na utawala limekamilika kwa asilimia 100 na limeongeza uwezo wa kuhudumia wanafunzi 1,620 kwa wakati mmoja, huku jengo la taaluma na utawala Kampasi ya Kigoma likifikia asilimia 98 na tayari linatumika. Kwa upande wa Mbeya, jengo la kumbi za mihadhara, maktaba na maabara ya kompyuta limekamilika kwa asilimia 100.

Katika eneo la wanafunzi, Prof. Pallangyo amesema idadi imeongezeka kutoka wanafunzi 24,494 mwaka 2022 hadi 37,397 mwaka huu wa taaluma, sawa na ongezeko la asilimia 52.7.

Ameongeza kuwa kati ya wanafunzi hao, 19,342 ni wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu kutoka HESLB, sawa na asilimia 51.7, huku wanafunzi 137 wa Kampasi ya Zanzibar wakinufaika na mikopo kutoka Zanzibar Higher Education Students’ Loan Board.

Aidha amebainisha kuwa TIA imeongeza programu za mafunzo kutoka 49 mwaka 2022 hadi 54, zikiwemo Shahada ya Maendeleo ya Biashara na Ujasiriamali pamoja na Shahada ya Uchumi na Fedha.

Amesema katika kipindi cha miaka mitano, TIA imekuwa na wahitimu wapatao 62,680, huku taasisi hiyo ikiendelea kuimarisha uwezo wa watumishi ambapo kwa sasa ina maprofesa tisa. Watumishi 78 wamefadhiliwa kwa ajili ya masomo ya shahada za juu, kati yao 48 wamehitimu na 30 wanaendelea na masomo ya PhD.

Ameongeza kuwa TIA imepanua pia upatikanaji wa programu za shahada ya uzamili kutoka Kampasi ya Dar es Salaam pekee hadi Kampasi za Zanzibar, Mbeya na Singida, huku Kampasi ya Mwanza ikitoa fursa hiyo kuanzia mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad